Genesis 8

Mwisho Wa Gharika

1 aMungu akamkumbuka Nuhu na wanyama wote wa porini na wa kufugwa waliokuwa naye ndani ya safina, akatuma upepo ukavuma katika dunia, nayo maji yakaondoka. 2 bZile chemchemi zilizo chini sana ya ardhi pamoja na malango ya mafuriko ya mbinguni yakawa yamefungwa nayo mvua ikawa imekoma kunyesha kutoka angani. 3 cMaji yakaendelea kupungua taratibu katika nchi. Kunako mwisho wa siku ya 150, maji yalikuwa yamepungua, 4 dkatika siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, safina ikatua katika milima ya Ararati. 5Maji yakaendelea kupungua hadi mwezi wa kumi, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana.

6Baada ya siku arobaini Nuhu akafungua dirisha alilokuwa amelifanya katika safina 7 ena akamtoa kunguru, akawa akiruka kwenda na kurudi mpaka maji yalipokwisha kukauka juu ya nchi. 8 fKisha akamtoa hua ili aone kama maji yameondoka juu ya uso wa ardhi. 9Lakini hua hakupata mahali pa kutua kwa kuwa maji yalienea juu ya uso wa dunia yote, kwa hiyo akarudi kwa Nuhu ndani ya safina. Nuhu akanyoosha mkono akamchukua yule hua akamrudisha ndani ya safina. 10Nuhu akangojea siku saba zaidi kisha akamtoa tena hua kutoka safina. 11Wakati hua aliporejea kwa Nuhu jioni, alikuwa amechukua katika mdomo wake jani bichi la mzeituni, lililochumwa wakati ule ule! Ndipo Nuhu akajua ya kuwa maji yameondoka juu ya uso wa dunia. 12Akangojea siku saba zaidi na akamtuma tena hua, lakini wakati huu hua hakurudi tena kwa Nuhu.

13 gKatika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza ya mwaka 601, wa kuishi kwake Nuhu, maji yalikuwa yamekauka duniani. Kisha Nuhu akafungua mlango wa safina akaona ya kuwa uso wa ardhi ulikuwa umekauka. 14 hKatika siku ya ishirini na saba ya mwezi wa pili dunia ilikuwa imekauka kabisa.

15Ndipo Mungu akamwambia Nuhu, 16 i“Toka ndani ya safina, wewe na mkeo na wanao na wake zao. 17 jUtoe nje kila aina ya kiumbe hai aliye pamoja nawe: Ndege, wanyama na viumbe vyote vitambaavyo juu ya ardhi, ili wakazae, na kuongezeka na kuijaza tena dunia.”

18 kKwa hiyo Nuhu akatoka nje pamoja na mkewe, wanawe na wake zao. 19Wanyama wote na viumbe vyote vitambaavyo juu ya ardhi na ndege wote, kila kitu kiendacho juu ya nchi, aina moja baada ya nyingine vikatoka katika safina, kila aina ya kiumbe, kimoja baada ya kingine.

Nuhu Atoa Dhabihu

20 lKisha Nuhu akamjengea Bwana madhabahu, akachukua baadhi ya wale wanyama na ndege wote walio safi, akatoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu. 21 m Bwana akasikia harufu nzuri ya kupendeza, naye akasema moyoni mwake, “Kamwe sitailaani tena ardhi kwa sababu ya mwanadamu, hata ingawa kila mwelekeo wa moyo wake ni mbaya tangu ujana. Kamwe sitaangamiza tena viumbe hai vyote kama nilivyofanya.”
22 n“Kwa muda dunia idumupo,
wakati wa kupanda na wa kuvuna,
wakati wa baridi na wa joto,
wakati wa kiangazi na wa masika,
usiku na mchana
kamwe havitakoma.”
Copyright information for SwhKC